Saturday, September 20, 2008

SAFISHA BOT




Hii ni kutoana nishaji jamani na ukiukwaji haki za wanawake yaani wengine wameamua kutoa wigi la urembo kujikinga na fedheha! Sijui wengine walikuwa na swaum?

TUHUMA za kuwepo kwa upendeleo wa watoto wa vigogo kwenye ajira za Benki Kuu ya Tanzania (BoT), zimesimamisha kizimbani wafanyakazi wanane ambao wameshtakiwa kwa kosa la kughushi vyeti.
Tuhuma dhidi ya watoto 16 wa vigogo ziliibuka wakati kashfa ya wizi wa fedha za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), ikiwa imeshamiri kiasi cha kusababisha aliyekuwa gavana, Daud Ballali kusitishwa mkataba wake na kufanyika kwa mabadiliko kadhaa kwenye uongozi wa chombo hicho nyeti cha fedha.
Na Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndulu, aliahidi kuzishughulikia tuhuma hizo wakati huo baada ya tuhuma hizo kushikiwa bango.
Jana, wafanyakazi wanane wa BoT, baadhi yao wakiwa wamejifunika nyuso kwa nguo na nywele za bandia, walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakishtakiwa kwa tuhuma za kughushi vyeti na kutoa hati za uongo.
Wafanyakazi hao, wengi wao wakiwa wanawake, ni Justina J Mungai, ambaye imeelezwa kuwa ni mtoto wa Joseph Mungai, ambaye amewahi kushika wizara tofauti ikiwemo ya elimu, Christina G Ntemi, Siamini Eddie Kombakono, Janeth John Mahenge, Beatha Constantine Massawe, Jacquiline David Juma, Philimina Philibert Mutagurwa na Amina Mohamed Mwinchumu.
Wafanyakazi hao walifikishwa katika mahakama hiyo saa 4.00 asubuhi na kusomewa shtaka mbele ya Hakimu Neema Chusi. Wakili wa serikali, Edgar Luoga, akisaidiana na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Abubakar Msangi, ndio walioongoza mashtaka hayo.
Washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kughushi vyeti vya kuhitimu kidato cha nne na kutoa hati za uongo kwa mwajiri wao, ambaye ni BoT.
Washtakiwa Mungai, Massawe na Mwinchumu, wanadaiwa kughushi vyeti hivyo mwaka 2001, wakati Ntemi, Kombakono, Mahenge na Mutagurwa wanadaiwa kughushi vyeti hivyo mwaka 2002. Wanadaiwa kughushi vyeti vya kuhitimu kidato cha nne na kutoa BoT hati za uongo, wakionyesha kuwa vimetolewa na Baraza la Mitihani la Taifa, wakati si kweli.
Ilidaiwa kuwa, Mutagurwa alighushi cheti hicho mwaka 2000.

1 comment:

Anonymous said...

Kabla ya kuanza na hawa mi napendekeza tungeanza na Wabunge!