Monday, September 22, 2008

SIMULIZI ZA MUSENDO 3

Musendo akiwa na mkewe, Paschalia na mtoto wao Joseph.

Katika sehemu ya pili ya simulizi ya mkasa uliomkuta Zephania Musendo, mhariri wa zamani wa gazeti la Family Mirror, tuliona maisha yake akiwa Gerezani, kuanzia Keko jijini Dar es Salaam hadi Mkuza mkoani Pwani. Pamoja na kero zote ndani ya gereza, leo anaelezea jambo moja lililomfurahisha na kumpa matumaini. Endelea...
SUALA la jinsi familia yake ilivyokuwa inaongozwa na mkewe asiyekuwa na kazi lilimsononesha sana hadi siku walipotembelewa na watu wa Chama cha Kusaidia Wafungwa (International Prisoners Relief Organisation). Watu hao walikuwa wamewapelekea misaada mbalimbali na katika mazungumzo yao walieleza kuwa pia wanasaidia familia za wafungwa.
“Habari hii ilinifurahisha sana. Wakati huo, nilikuwa na taarifa kuwa mtoto wangu aliyekuwa kidato cha tatu, alikuwa amefukuzwa shule kwa kukosa ada, hivyo niliwaomba watu hao wamsaidia arejee shule. Walikubali, wakanieleza utaratibu. Niliandika barua ikapitishwa kwa bwana jela, nikajenga matumaini, lakini mpaka ninatoka jela jana (Jumanne) sikujua iliyeyukia wapi, lakini kikubwa nilifurahi kuona angalau kuna chama kama hicho cha kusaidia wafungwa, kwani wengi wanahitaji msaada mno.”
Musendo anasema pamoja na furaha yake hiyo kuyeyukia gerezani, baadaye alipata fursa nyingine, aliandika barua kwa meneja wa benki na kumpatia mkewe ili aruhusu pesa zitolewe kwenye akaunti yake, ili mtoto wake huyo apate ada na kurudi shule.
“Nashukuru sana meneja yule alielewa na mtoto akalipiwa,” anasema Musendo.
Kitu kilichomsumbua ni mwishoni wakati anakaribia kumaliza kifungo chake, “unajua unawekewa lebo kifuani kuonyesha siku ya kuingia na ya kutoka. Kadri siku zilivyokuwa zinakaribia kufika, ndio ilikuwa inaonekana ni mbali zaidi na maisha nayaona kama hayaendi.”
Anasema anamshukuru Mungu siku hiyo ilifika wiki hii. Licha ya matatizo ya maradhi yaliyokuwa yanamsumbua alitoka gerezani salama na kufurahi kumwona mkewe na ndugu kadhaa wakiwa wamefika gerezani hapo kumlaki na kumchukua, lakini anatambua kuwa ana kazi nzito ya kufanya ili kuweka maisha yake sawa.
“Kwa sasa ninajua ninayo majukumu mazito, kwani kukaa jela kwa miaka mitatu vitu vingi vinarudi nyuma, natamani nipate kazi kwanza na baadaye nikipata nafasi nitaandika kitabu kuhusu mambo ya jela, hasa mateso wanayopata watu wenye Ukimwi.”
Lakini sasa Musendo ambaye yuko huru na amerejea nyumbani kwake Kawe jijini Dar es Salaam, anasikitishwa na hali aliyoikuta nyumbani kwake.
“Kuna mabadiliko makubwa sana nimeyakuta hapa nyumbani, kama ile migomba haikuwapo sasa naona ni mingi na watoto wamekua,” anasimulia huku akionyesha migomba hiyo.
Kinachomsikitisha zaidi Musendo ni jinsi alivyokuta nyumba aliyokuwa akiijenga, ndimo anaishi sasa kabla haijakamilika sawasawa na hivyo anaona kuwa kwa miaka mitatu aliyoipoteza jela angekuwa amefanya jambo la maana zaidi.
Musendo mwenye watoto watano wakiwamo wa kike wawili, anadhani kama angekuwa huru watoto wake wasingesoma kwa shida kama ilivyokuwa wakati akiwa jela.
Anasema kijana wake wa kwanza ni fundisanifu na yuko jijini Dar es Salaam, wakati wa pili ni mwanafunzi wa Stashahada ya Juu katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), mwingine wa kike yuko tu nyumbani. Binti yake mwingine sasa anasoma sekondari. Mtoto wake wa mwisho, Joseph ndio amefanya mtihani wa darasa la saba.
Joseph aliachwa akiwa darasa la nne wakati baba yake anaenda jela na sasa amekuwa kijana mkubwa tu wa miaka 14. “Nilikuwa mdogo lakini nilijua kuwa baba amefungwa, nilipata habari kwenye gazeti.”
Joseph anaeleza kuwa ilikuwa vigumu kuamini kuwa baba yake hatamuona tena na kikubwa lichofanya ni kujifungia chumbani na kulia. “Nilikuwa nalia na kila siku nilikuwa namwombea kwa Mungu ili aweze kutoka,” anasema mtoto huyo.
Ingawa Jumanne iliyopita hakwenda kumwona baba yake wakati akitoka jela, lakini alijua kuwa angerejea siku hiyo. “Nilifurahi nilipopata taarifa kama angerejea na nikajua kuwa atanisaidia kuendelea na masomo kwa kuwa nimemaliza la saba.”
Lakini kikubwa ambacho kimemshangaza Musendo ni kukutana na mjukuu wake ambaye ni mtoto wa mwanae wa kiume. Mjukuu huyo amepewa jina la babu yake. “Huyu mtoto anaitwa Zephania ndio surprise nyingine niliyoikuta nyumbani”.
Mkewe, Pachalia anasema kuwa kufungwa kwa mumewe ni kitu kilichomuumiza sana kwa kipindi chote alipokuwa ndani, “sasa hivi nimefurahi sana kuwa naye tena nyumbani, ni kama siamini,” alisema kwa furaha.
Akikumbukia ayaliyopita, anasema kuwa siku ilipotolewa hukumu dhidi ya mumewe, alilia sana na hakujua kitu cha kufanya kwani kwa wakati huo alikuwa mama wa nyumbani tu. Pamoja na balaa yote hiyo lakini pia imemsaidia kuwa mkakamavu zaidi na aliweza kufanya mambo yaende kwa kiasi kikubwa sana.
Paschalia anasema kuwa alikuwa akimwomba Mungu na kumpa moyo mumewe kila mara alipomtembelea jela. “Nilimwambia Mungu atakujalia na utatoka salama na kurejea katika familia. Nafurahi Mungu alisikia maombi yangu na amerudi salama.”
Musendo anaeleza kuwa hakutegemea kuwa mkewe angeweza kufanya yote aliyoyafanya na anashukuru na kumpongeza, kwamba pamoja na baadhi ya mambo kuharibika, lakini familia iko salama na yeye ana afya njema.
“Ninachotarajia sasa ni kupata kazi nikishapata kazi na kuanza kuhudumia familia yangu kama zamani najua tutaweza kuweka vitu vingi sawa.”
“Sasa hivi natakiwa niweze kumudu familia yangu, nahitaji regular income (kipato kisichotetereka) ili maisha yaendelee, hivyo ninachohitaji ni kupata kazi tu na nitaendelea kuwa mwandishi wa habari.”
Kauli hiyo ya Musendo anaitoa huku akisisitiza kuwa kwa miaka ya sasa kazi ya uandishi inakuwa na changamoto nyingi.
“Kwa kuwa mwandishi kwa sasa atakuwa na vitu vingi kwa kuwa tunaandika mambo yanayofichua maovu, na hii haifurahishi wakubwa,” anasisitiza.
Anasema kwa kuwa aliingia katika taaluma hiyo basi atabakia nayo kwa kuwa ukiamua kuwa mwandishi wa habari chochote kinachokupata inakuwa ni sehemu ya kazi na funzo kwa wengine. “Nina mpango wa kutunga kitabu lakini pia nitaendelea na kazi ya uandishi wa habari.”
Ana wito gani? Musendo anawaasa waandishi wa habari kuwa makini katika kazi zao na wahudumie jamii kwa kutoa vilio vyao. “Mbona wewe ulipigwa na askari magereza, hizo ni challeges tulizonazo kwenye kazi yetu. Lakini si bado unaendelea?”.
Mwisho




No comments: