Saturday, September 20, 2008

SUMULIZI ZA MUSENDO 2

Roho iliniuma sana, nikamshukuru Mungu

Katika sehemu ya kwanza ya simulizi ya mkasa uliomkuta Zephania Musendo, mhariri wa zamani wa gazeti la Family Mirror, tuliona jinsi mwandishi huyo mkongwe alivyosimulia mkasa mzima uliosababisha ahukumiwe kwenda jela kwa miaka mitano, kifungo alichokitumikia kwa miaka mitatu. Leo anasimulia jinsi alivyoingia gerezani kuanza maisha ambayo hakuwahi kuyaota. Endelea...

BAADA ya hakimu Suma Seme kutamka kuwa amehukumiwa kwenda jela miaka mitano, Zephania Musendo anasema hakuamini macho yake! na alipata mshtuko mkubwa kwani hakutarajia kuwa angefungwa kutokana na imani yake kuwa mkasa mzima ulikuwa wa kutengeneza.
Hakuamini, lakini alilazimika kukubali matokeo ya hukumu hiyo iliyotolewa asubuhi ya Mei 17, 2005."Sikuamini na hata mke wangu Paschalia na ndugu zake hawakuamini na nikawaona wanaangua kilio," anasema.
Hali ilikuwa hivyo kwa mkewe.“Sikuamini kwa kuwa nilijua sasa anaenda jela na sitakuwa naye tena,” anasema mkewe. “Mpaka alipotolewa chumba cha mahakama na kuwekwa lock up (rumande) ya pale mahakamani na maaskari wakaniambia kuwa ‘huyu si wenu tena, ni wa kwetu’.
Roho iliniuma sana, nikamshukuru Mungu.”Baada ya kutolewa hukumu hiyo, Musendo anasema alichukuliwa na kupelekwa katika gereza la Keko jijini Dar es Salaam, ambako alianza kutumikia kifungo hicho na maisha mapya ya jela.
“Tulipofika pale gerezani, wana utaratibu wa watu kupekuliwa hasa wafungwa wapya, kwa hivyo tulivuliwa nguo zote kwa ajili ya upekuzi,” anasema.Anaeleza kuwa kitendo cha kuvuliwa nguo zote mbele ya wafungwa wengine ndicho kilikaribisha maumivu mengine kwani kuna baadhi ya wafungwa aliokuwa nao walikuwa na umri wa watoto wake, lakini hakuwa na uhuru tena, ilimlazimu kufuata amri.
“Maisha ya Keko yalikuwa ni ya msongamano na niliona mambo mengi yanayohusu wafungwa, mbayo nilikuwa nasikia sikia tu, lakini nilikuja kuamini kuwa ilikuwa ni kweli”.
Katika jela ya Keko, alikaa kwa muda wa mwezi mmoja inagawa kulikuwa na msongamano wa watu lakini kulikuwa na matandiko mazuri na walilala kwa kujipanga ili kuweza kutosha katika chumba kidogo.Baadaye alihamishiwa jela ya Mkuza, iliyoko Kibaha mkoani Pwani, ambako kwa maoni yake kuna tofauti kubwa na jela ya Keko, kwani haina ngome kubwa kama ilivyo kwa jela nyingine kubwa, Magodoro yamekwisha na hali si nzuri sana.
“Kuna wakati roho inauma kwani tokea magodoro yaletwe mara ya kwanza hayajabadilishwa na vimebakia vipande vidogo ambavyo mtu unavikusanya na kuunganisha mpaka upate sehemu ya kulala.”
Musendo anasimulia kuwa alipofika jela alikutana na watu wengi ,wakiwamo majambazi, vibaka na wengine ambao wamefungwa kwa mashtaka ya uhalifu au kesi za kusingiziwa na kubambikwa, lakini wote walikuwa wakitumikia vifungo vyao.
Anasema kuwa chakula jela kilikuwa cha kawaida, kwani walikuwa wakila ugali na maharage kila siku, isipokuwa Jumamosi walipokuwa wakila wali na maharage wakati Jumapili kulikuwa na nyama.
“Kwenye chakula ndio hivyo tena, unaweza kukutana na wadudu katika maharage au unga, utakula tu utafanyaje?”Kutokana na kuwa na matatizo ya kiafya hasa kwa magonjwa wa moyo na kisukari ambayo yalikuwa yakimsumbua kwa muda mrefu kabla ya kufungwa, alilazimika kuomba kupatiwa chakula maalum (special diet), lakini ilishindikana kwani aliambiwa kuwa jela hiyo haikuwa na utaratibu kama huo.
“Mkuu wa Gereza alinieleza kuwa hakukuwa na special diet hivyo aliniruhusu kama ndugu zangu wangeweza kuniletea sawa, kwa hivyo nikawa naletewa samaki, matunda na karanga kwa muda fulani.”
Kuhusu maziwa mbayo aliomba, aliambiwa kuwa kwa kuwa ng’ombe wa gereza walikuwapo angetakiwa kulipiwa bili na ndugu zake na hivyo gereza kumpatia.
“Lakini baadaye Bwana Jela alinionea huruma kwa kujua kuwa mimi ndio nilikuwa kichwa cha familia wasingemudu kulipia kwa muda wote, akaamua nipewe bure, namshukuru sana.”
Siku iliyomuumiza
Akisimulia siku mbayo imemuumiza na kumfedhehesha alipokuwa jela, alisema kuna siku upekuzi wa kawaida katika gereza ulikuwa ukifanyika na wafungwa wote walitakiwa kuvua nguo zote na kuchuchumaa.
“Tulitakiwa kuruka kichura, nilipojaribu kuruka na hii hali yangu (ya ugonjwa) nilidondoka chini.
Nilitarajia kuwa mtu wa kwanza kunisaidia angekuwa daktari wa jela, ambaye alikuwepo sehemu hiyo.
Lakini hakufanya lolote na niliachwa nikigalagala chini.”“Roho iliniuma sana kwa kuwa Bwana Jela pia hakujali bali alisema hakuna taabu na kuwa mimi nilikuwa nazuga tu”.Anasema, alifikiria pale alipokuwa amelala akiwa uchi, kila mtu alikuwa akimwangalia, na kwa kuwa gereza hilo halikuwa na ukuta, basi hata watu wakiwamo wanafamilia wa askari waliweza kumwona.
“Sitasahau siku hiyo kamwe.”
Maisha ya dini gerezani
Musendo anasema, kwa kawaida walikuwa wakiamka mapema asubuhi ili kupeana nafasi ya kuabudu ndani ya seli zao, “Kwanza tulikuwa tunawapisha Waislamu ambao walikuwa wananza sala zao mapema saa 11 alfajiri.
Baadaye tunakuja Wakristo na kulikuwa na watu waliokuwa wanatuongoza”.Anasema pamoja na kuwa watu walikuwa wakisali ndani ya seli hizo, bado kuna wengine kwa hiyari yao walikuwa hawaabudu na hawataki kabisa kusali.
“Ingawa sikuwa mtu wa dini sana, lakini nilikuwa nasali kila siku na wenzangu na tulikuwa tunapeana masomo ya biblia. Pia kuna watu wa Sabato walikuwa wanakuja kufanya sala na kutugawia vitu mbalimbali kama sabuni, ndala, nguo na hata viatu.”
Baada ya sala, Musendo anaeleza walikuwa wananatolewa nje na kuhesabiwa, na ulikuwa utaratibu wkawaida na baadaye walikunywa uji na kupangiwa majukumu, ikiwamo kutafuta kuni, kwenda shambani, bustanini, kufyatua matofali na kazi nyingine za ndani ya gereza.
Baada ya kutawanyika na kwenda maeneo ya majukumu, wote huendelea na kazi hadi saa nane mchana ambapo hurejeshwa gerezani kupata mlo wa mchana na baadaye saa 10 kufungiwa katika seli, kuhesabiwa na kuendelea na mambo mengine.
“Wengine walikuwa wanapenda kucheza karata, ingawa sina hakika kama zinaruhusiwa na wengine walikuwa wanapiga ‘story’ na kuvuta sigara tukisubiri usiku ili siku ipite, ingawa tulikuwa tunafungiwa mapema lakini ilikuwa vigumu kulala saa 10 jioni.”
Anaeleza kuwa cha kushangaza pamoja na kupekuliwa kwa uhakika lakini vitu mbalimbali visivyoruhusiwa vilikuwa vinapatika ndani ya jela, zikiwamo sigara na hata bangi, “Sijui ilikuwaje lakini nadhani kuna syndicate (njama) kubwa ya biashara hizo inawezekana inahusisha hata maaskari.
”Musendo anasema bahati yake nzuri aliheshimika sana, na watu walikuwa wakimpenda kwani alikuwa anajua vitu vingi, na hivyo kumfanya awe na mahusiano mazuri hadi kuwa kiongozi wa wafugwa (mnyampala) wa kuwasimamia wenzake.
Lakini kuitu kilichokuwa kikimsumbua zaidi ni kuishi huko huku kijua kuwa mkewe hakuwa na kazi, na alikuwa na watoto watano wanaomtegemea. Hali hiyo ilimkera na kumsononesha, ingawa mkewe alijaribu kumweleza kuwa mambo yanaenda sawa kila alipomtembelea.
Anasema hali hiyo ilimsononesha sana hadi siku moja walipotembelewa na watu wa Chama cha Kusaidia Wafungwa (International Prisoners Relief Organisation ) ambao misaada mbalimbali na kuwaahidi kuwa wanazisaidia hata familia za wafungwa.“Nilikuwa na taarifa kuwa mtoto wangu aliyekuwa kidato cha tatu, alikuwa amefukuzwa shule kwa kukosa ada na niliwaomba watu hao kama wangeweza kumsaidia ili arejee shule.
Wakanieleza utaratibu, nikaandika barua, ikapitishwa na bwana jela lakini mpaka natoka jana sijajua ilikwamia wapi?, Lakini kikubwa nilifurahi kuona angalau kuna chama kama hicho cha kusaidia wafungwa, kwani wanahitaji msaada mno.”
Musendo anasema pamoja na kutokea hivyo baadaye alimwandikia barua meneja wa benki na kumpatia mkewe, ili aruhusu pesa zitolewe kwenye akaunti yake ili isaidie ada ya mtoto.
“Nashukuru sana meneja yule alielewa na mtoto alilipiwa.Kwa mujibu wa Musendo, kitu kilichomsumbua ni mwishoni wakati anakaribia kumaliza kifungo chake, “Unajua unapofungwa unaandikwa kifuani siku ya kuingia na siku ya kutoka.
Sasa kadri siku zilivyokuwa zinakaribia kufika ndio ilikuwa kama ni mbali zaidi na maisha nayaona kama hayaendi.”Anasema anamshukuru Mungu siku hiyo ilifika wiki hii na pamoja na kuwa na matatizo ya maradhi yake, ametoka salama na alifurahi kuona mkewe na ndugu kadhaa wakiwa wamemfuata kumchukua.
Alimshukuru Mungu na kuona kuwa ana kazi nzito ya kufanya na kuweka maisha yake sawa.
“Kwa sasa ninajua nina majukumu mazito kwani kukaa jela miaka mitatu ,vitu vingi vinarudi nyuma, natamani nipate kazi kwanza na baadaye nikipata nafasi nitaandika kitabu kuhusu mambo ya jela hasa mateso wanayopata watu wenye Ukimwi”.
Kesho simulizi hili litaendelea sehemu ya tatu, kuhusu hali aliyoikuta nyumbani baada ya kumaliza kifungo chake

No comments: