Thursday, September 03, 2009

ABRAMOVICH NDANI YA BONGO




MMILIKI wa Klabu ya soka ya Chelsea, inayoshiriki katika ligi kuu ya Uingereza, Roman Abramovich ametua mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kupanda Mlima Kilimanjaro.
Abramovich, ambaye ni tajiri wa Kirusi atakuwepo nchini hadi Septemba 11, mwaka huu atakapoondoka kurudi Uingereza anakoishi.
Tajiri huyo wa klabu ya Chelsea alikuja jana saa 1 jioni akiwa na watu 6 na amefikia katika Hoteli ya River Trees Country Inn, iliyopo eneo la USA River nje kidogo ya Mji wa Arusha ambayo hivi sasa haruhusiwi mtu mwingine kuingia katika hoteli hiyo.
Meneja wa Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ,Said Mzava jana jioni alisema Abramovic amefurahi kufika Tanzania kuona mlima Kilimanjoro na vivutio vingine vya utalii.
Huku akiwa analindwa na walinzi watatu, Abramovich alikataa kuzungumza na vyombo vya habari akisema kuwa amechoka anahitaji kupumzika.
Abramovich ambaye amekuja na ndege yake binafsi aina ya Boeing 767, pia alikutana na kusalimiana na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara nchini, Cyril Chami aliyekuwepo uwanjani hapo kwa shughuli zake binafsi.

No comments: