Monday, March 08, 2010

MREMA TAJIRI


MWENYEKITI wa TLP, Augustine Mrema, ambaye katika siku za karibuni amekuwa akizungumzia sana masuala ya baadhi ya viongozi wa CCM, jana alitamba kuwa ana utajiri wa Sh37 milioni kwenye akaunti yake na hivyo ni tajiri kuliko Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Alikuwa akijibu kauli iliyotolewa na Spika Samuel Sitta ambaye alimuelezea waziri huyo wa zamani wa mambo ya ndani kuwa amefilisika kisiasa na kifedha na ndio maana anahaha kujikwamua kwa kuipigia debe CCM.
Sitta, ambaye ameongoza kipindi cha mwisho cha uspika wake kwa mapambano dhidi ya watu aliowaita maadui wake wa kisiasa, alidiriki kumuelezea Mrema kuwa amefilisika na kwamba huenda anapata fedha kutoka chama hicho tawala.
Sitta alitoa tuhuma hizo nzito baada ya Mrema kuitisha mkutano na waandishi wa habari na kumtuhumu spika kuwa ana makundi ndani ya Bunge na kwamba anaendelea kuzungumzia sakata la utoaji zabuni ya kufua umeme wa dharura kwa Richmond Development LLC kwa kuwa mjadala huo ulishafungwa na Bunge.
Jana Mrema alikanusha tuhuma zote hizo na kudai kuwa yeye hajafulia wala hajafilisika kisiasa na kifedha na kwamba hajachanganyikiwa wala kuhongwa na CCM ili akipigie debe na akamtaka Spika Sitta atoe ushahidi wa tuhuma zake.
Pia Mrema alitangaza kuwa atamfikisha mahakamani Sitta kwa madai kuwa amemkashfu na kumvunjia heshima mbele ya jamii na pia atamshtaki kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa kwa kuwa amevunja kanuni za vyama vya siasa kwa kutoa maelezo ya uongo dhidi yake.
"Mimi nilimuonya mheshimiwa spika kwamba aache kuwa na makundi ndani ya Bunge na asiendelee kulalamikia suala la Richmond kwa sababu mjadala huo ulishafungwa na Bunge. Na kama haridhiki yeye pamoja na wenzake wajiondoe CCM kama nilivyofanya mimi mwaka 2005,"alisema Mrema katika mkutano wake na waandishi jana.
"Lakini badala ya kujibu hoja, Mheshimiwa Sitta akaamua kunikashfu na kunitukana mimi kama mtu binafsi, jambo ambalo ni kinyume cha kanuni za vyama vya siasa zilizopitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa mwaka 2007, Ibara ya 5(d) inayotaka kutotoa maneno yoyote au maandishi ambayo ni ya uongo kuhusu mtu yeyote au chama chochote cha siasa."
Akifafanua kuhusu tuhuma hizo, Mrema alisema kifedha hajafilisika bali yeye ni tajiri kuliko hata Pinda kwa kuwa anamiliki Sh.37.75 milioni kwenye akaunti yake.
Mimi sijafulia. Kufulia kwa lugha ya mitaani ni kufilisika hata kukosa fedha ya Chakula. Namhakikishia mheshimiwa spika kwa kuwa sijafulia kama anavyodai kwani nina uwezo wa kujilisha na familia yangu pamoja na kusomesha watoto wangu na kujitibu ninapoumwa bila ya msaada wa mtu yeyote," alisema Mrema.
"Nimefanya kazi serikalini kwa zaidi ya miaka 30 nikiwa ofisa wa Usalama wa Taifa, mbunge, waziri na baadaye naibu waziri mkuu

No comments: